Huwa inatokea sana pale mwanamke
anamfumania mume au mpenzi wake, kitakachotokea kama si kumpiga mwanamke
aliyemfumania na mumewe, basi atamporomoshea matusi au kumlaumu sana.
Si hivyo tu, hata pale mwanamke anapopata fununu kwamba mume wake au
mpenzi wake anatoka na mwanamke fulani, sio kwamba atamkabili mumewe au
mpenzi wake kutaka kujua ukweli wa jambo hilo, bali atakachofanya ni
kumkabili mwanamke huyo iwe ni moja kwa moja au kwa kutumia wanawake
wenzie ili wamfikishie ujumbe huyo mwanamke anayemtuhumu.
Je ni kwa nini hali hiyo hutokea……?
Hapa chini nitajaribu kudadavua sababu
kadhaa zinayowafanya wanawake kukimbilia kuwalaumu wanawake wenzao
wanaowafumania na waume zao:
1. Kupinga kuhusu jambo hilo - Sababu
kubwa inayowafanya wanawake kuwalaumu wanawake wenzao pale
wanapowafumania na wenzi wao ni kwa kuwa ni rahisi zaidi kukabiliana na
wanawake wenzao kuliko waume zao. Ingawa inawezekana mwanamke akawa
anahisi kwamba mwenzi wake anatoka nje, lakini mara nyingi wanawake
hupinga uwezekano wa jambo hilo kuwepo. Hiyo ni kwa sababu wakati
mwingine mwanawake hutokea kumuamini mwenzi wake kupita kiasi, hivyo
kutotaka kuruhusu mawazo ya aina hiyo yatawale kichwa chake. Hivyo basi
kuwalaumu wanawake wenzao ni rahisi zaidi kuliko kujikagua na kuangalia
kama mahusiano yake na mwenzi wake iwapo yana tatizo. Lakini kinyume
chake huamini kwamba ni lazima mwanamke huyo ndiye aliyemshawishi mwenzi
wake mpaka akakubali kutoka naye. Pia huamini kwamba kama mwanamke huyo
asingejirahisisha kwa mwenzi wake, isingekuwa ni rahisi kwake
kutongozwa na kukubali, ni lazima kulikuwa na aina ya kujirahisisha ili
kumshawishi mwenzi wake atoke naye. Lakini pia wanawake wengi huchukulia
kitendo cha mwenzi wake kutoka nje ni kama wamechokwa na sasa waume zao
hawawataki. Hakuna mtu anayependa kuachwa, hivyo ni rahisi zaidi
kuwakabili au kuwalaumu wanawake wenzao kuliko waume zao au hata
kujilaumu kutokana na mahusiano mabovu na wenzi wao
2. Kuhisi kusalitiwa kama mwanamke - Kwa
kawaida wanaume wana tabia ya, "kila mtu na lwake," tofauti na
wanawake, wao wana tabia ya ushirikiano na wanaamini kwamba madhila ya
mwenzake ni ya kwake pia. Hivyo kitendo cha kugundua kwamba mwanamke
mwenzake amemsaliti jambo hilo humuumiza sana. Ingawa wanawake wanajua
wazi kwamba mwanaume kutoka nje ni jambo rahisi na linalowezekana sana
kutokana na asili ya wanaume, lakini huamini kwamba wanawake ni wamoja
na hawapaswi kusalitiana wao kwa wao.
3. Kutafuta shabaha dhaifu –
Baadhi ya wanawake huona ni rahisi zaidi kuwakabili wanawake wenzao
kuliko waume zao. Hususan kama anamuogopa mumewe. Kama mwanaume ana
historia ya unyanyasaji na upigaji wa wanawake halafu ikatokea mwanamke
akagundua kwamba mwenzi wake huyo anatoka nje, kamwe haitatokea mwanamke
huyo kumkabili mumewe. Kitakachotokea ni kwa mwanamke huyo kumkabili
mwanamke mwenzie akiamini kwamba shari haitakuwa kubwa ukilinganisha na
ya mumewe. Pia kuna baadhi ya wanaume wana tabia ya uzinzi na mkewe au
mpenzi wake anajua kabisa kwamba ni vigumu kwake kubadilika. Hapa
atakachofanya mwanamke huyo ni kukimbizana na wanawake wenzie anaowahisi
kuwa wanatoka na mumewe au mpenzi wake huyo ili kuwapa ujumbe kwamba
anawafahamu na anawafuatilia, akiamini kwamba watamwacha mumewe, hivyo
haoni sababu ya kumkabili mpenzi wake.
4. Wanawake hawapendi kupoteza
– Inapotokea mwanamke amegundua kwamba mpenzi wake anatoka
nje, hujiwa na mawazo mengi sana, miongoni mwa mawazo hayo ni(i).
Je kuna jambo amemkosea huyo mwenzi wake mpaka kufikia kiasi cha
kumsaliti? (ii). Je Mwanamke huyo aliyotoka na mwenzi wake ni mzuri
kiasi gani, au amemzidi na kitu gani hasa? Kama ikitokea akimkabili
mwenzi wake kutaka kujua ukweli kuhusu jambo hilo halafu huyo mpenzi
wake akasema hampendi huyo mwanamke na wala hamtaki ila huyo mwanamke
ndio anajipendekeza kwake, hapo itakuwa ni rahisi kwake kumkabili huyo
mwanamke kidudu mtu, kwani mpaka hapo atakuwa amethibitisha kwamba yeye
ni mshindi kwani mwenzi wake yuko upande wake na si wa hawara yake.
5. Amepanga kuishi na mwenzi wake mpaka
kifo kiwatengenishe- Kuna wanawake ambao wamejitolea na kujiapiza
mioyoni mwao kwamba wao na wenzi wao wataishi pamoja labda tu kifo ndio
kitawatenganisha. Hata kama itatokea ajue dhahiri kwamba mwenzi wake
anatoka nje na amejitahidi kulijadili jambo hilo na mwenzi wake lakini
haoneshi dalili za kuacha mchezo wake huo, basi ni rahisi sana kwa
mwanamke kuhamishia hasira zake kwa wanawake anaowahisi kuwa wanatoka na
mwenzi wake. Ukweli ni kwamba hakuna mwanamke anayependa kufanywa
mjinga katika uhusiano, hata kama kiukweli watu waliomzunguka humwona
kuwa ni mjinga kutokana na vitendo anavyofanyiwa na mwenzi wake, lakini
anashindwa kuchukua maamuzi magumu. Hivyo basi ili kuondoa hiyo dhana ya
kuonekana mjinga hukimbilia kuwakabili wanawake wenzie anaohisi
wanatoka na mwenzi wake.
6. Anatoka na mwanamke anayemfahamu
vizuri sana – Hii ni moja ya sababu nzuri inayoweza kutumiwa
na mwanamke kuhalalisha kwamba ni kwa nini amkabili manamke mwenzie
badala ya mwenzi wake. Kama inatokea mwanaume anatoka nje na rafiki wa
karibu wa mkewe, mfanyakazi mwenzie au kibaya zaidi atoke na ndugu wa
karibu, hapo ni dhahiri mwanamke anayo kila sababu ya kumlaumu mwanamke
mwenzie. Na si hivyo tu kama inatokea anatoka na ndugu wa karibu labda
tusema dada au mdogo wake wa kike, huwa inawaumiza sana wanawake na
uwezekano wa ndugu kusambaratika ni mkubwa, kwani anashindwa kuamini
kile kilichotokea. "Yaani hata ndugu yangu mwenyewe
ananisaliti……" anaweza kujiuliza. Na kama ni shoga
yake ndio kabisaa itamuuma zaidi. Ikumbukwe kwamba wanawake huwa
wanashirikiana hisia. Kama inatokea anagundua kwamba yule rafiki
aliyemuamini na ambaye anamshirikisha katika madhila yake kwa kumweleza
matatizo yake na mwenzi wake, ndiye anayetoka na mpenzi wake, jambo hili
huwaumiza sana wanawake kihisia
No comments:
Post a Comment